Mwenge wa Uhuru 2023 umeanza kukimbizwa Leo Mei 6 ukitokea Mkoani Iringa ambapo unatarajia kupitia jumla ya miradi 68 yenye thamani ya Tsh. zaidi ya Bil.12.
Ukiwa Mkoni humo Mwenge wa Uhuru unatarajiwa kukimbizwa katika Halmashauri zote tisa ambapo leo umekamilisha mbio zake katika Halmashauri ya Mlimba iliyopo Katika Wilaya ya Kilombero.
Ndani ya Halmashauri hiyo Mwenge wa Uhuru umepitia miradi mbalimbali ikiwa ni pamoja na mradi wa kituo cha Afya Chita
Akizungumza na wananchi wa eneo la miradi mkimbiza Mwenge wa Uhuru Kitaifa ndugu Abdallah Shaib Kaimu amesisitiza watendaji mbalimbali kukamilisha nyaraka za malipo yanayofanywa kwa mafundi zikiwemo nyaraka za ujenzi wa majengo yote ya serikali.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa ndugu Abdallah Shaib Kaimu akiweka jiwe la msingi ujenzi wa jengo la mama na mtoto pamoja na upasuaji katika kituo cha Afya Chita.
Ndg. Abdallah Shaib ametoa rai hiyo wakati akiweka jiwe la msingi ujenzi wa jengo la mama na mtoto pamoja na jengo la upasuaji.
Awali mara baada ya kuupokea mwenge wa Uhuru Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma Mwassa amesema Mwenge utakimbizwa katika Halmashauri zote tisa za Mkoa wa Morogoro kwa umbali wa Km 1,588 na utapitia jumla ya miradi ya maendeleo ipatayo 68 yenye thamani ya Shilingi za kitanzania 12,170,922,197.46.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma Mwassa akipokea Mwenge wa Uhuru kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe. Halima Dendego baada ya kukamilisha mbio zake Mkoani Iringa.
Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa ameongeza kuwa Kati ya miradi 68 itakayopitiwa na Mwenge wa Uhuru, miradi 5 itafunguliwa, miradi 19 itazinduliwa, miradi 20 itakuwa ya kuonwa na miradi 24 itawekewa mawe ya msingi.
Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Fatma Mwassa akizungumza na Viongozi na wananchi ambao wamejitokeza kuupokea Mwenge wa Uhuru ukitokea Mkoani Iringa.
Miradi yote hiyo imefanikiwa kufika hapo ilipofikia kutokana na ushirikiano mzuri uliopo baina ya Serikali, Wananchi na Wadau mbalimbali wa maendeleo.
Mradi wa madarasa matano katika Shule ya Sekondari Ngai ni miongoni mwa miradi iliyopitiwa na Mwenge wa Uhuru.
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Kituo cha Afya Chita Dkt. Karim Msola ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kufanikisha ujenzi wa Wodi ya mama na mtoto pamoja na jengo la upasuaji ambalo litaokoa maisha ya wanawake wajawazito na watoto zaidi ya 20,000 ambao walikuwa wanatembea umbali wa zaidi ya kilometa 21kufuata huduma za Afya katika vijiji vingine.
Viongozi mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya za Mkoa wa Morogoro, Wakurugenzi wa Halmashauri, na Wajumbe wa Sekretarieti ya Mkoa wa Morogoro wameshiriki mapokezi ya Mwenge wa Uhuru.
MWISHO.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.