Vyama vya ushirika hapa nchini vimetakiwa kuendana na maendeleo ya sayansi na teknolojia duniani, ambapo matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasikiano - TEHAMA yanatajwa kuwa ni njia bora ya kurahisisha utendaji kazi na kuongeza tija katika maendeleo ya vyama hivyo.
Hayo yameelezwa na Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Morogoro, Bi. Cesilia Filimin, wakati akifungua Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Mkoani humo, lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mbaraka Mwinshehe uliopo Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro.
Akifafanua zaidi, Bi. Cesilia amesema kuwa vyama hivyo vinapaswa kuachana na matumizi ya mifumo ya analojia, hususan matumizi ya karatasi katika utunzaji wa takwimu na taarifa nyingine muhimu, badala yake vigeukie mifumo ya kidijitali ambayo ni rahisi na ya haraka ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi.
"Dunia kwa sasa inaelekea kwenye matumizi makubwa ya TEHAMA; zama za matumizi ya karatasi zimepitwa na wakati. Jikiteni kwenye dijitali," amesema Bi. Cesilia Filimin.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Maendeleo ya Ushirika Mkoa wa Morogoro, Bw. Iddi Bilali, amesema jukwaa hilo limekuwa likifanyika kila mwaka na limekuwa na mafanikio makubwa katika kubadilishana uzoefu, kujadili changamoto na mafanikio ya vyama, pamoja na kuimarisha utendaji kazi na uendeshaji wake.
Kwa upande wao wanachama wa vyama vya ushirika akiwemo Bi. Florentina Kachelwa amesema kabla ya kujiunga na vyama hivyo, wakulima walikuwa wanakumbwa na changamoto za upatikanaji wa pembejeo za kilimo, mbolea na mbegu bora. Hata hivyo amesema baada ya kujiunga na vyama hivyo, baadhi ya changamoto hizo zimeanza kutatuliwa.
Hata hivyo ameiomba serikali kuendelea kuunga mkono juhudi za kutatua changamoto hizo ili kuwawezesha wakulima wanaotegemea vyama vya ushirika kuendesha maisha yao kwa ufanisi.
Mwisho.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.