Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Kighoma Malima, ameendelea kubeba maono ya kukuza sekta ya kilimo katika mkoa huo kwa kulima mazao ya kimkakati yakiwemo karafuu, kakao, parachichi, chikichi na kahawa, ambayo amesema yatachochea ukuaji wa uchumi ndani ya Mkoa na Taifa.
Mhe. Malima amebainisha hayo Juni 26, 2025, wakati akifungua mkutano wa Baraza la Biashara la Mkoa wa Morogoro uliofanyika katika Hotelli ya Morena halmashauri ya Manispaa ya Morogoro na kujumuisha viongozi ngazi ya mkoa, wilaya, makampuni binafsi na wajasiriamali.
Mhe. Malima amesisitiza kuwa huu ni wakati muafaka kwa Mkoa huo kujitangaza na kutambulika kitaifa na kimataifa kupitia sekta ya kilimo, hasa kilimo cha kisasa cha mazao ya kimkakati yana soko ya kimataifa huku akibainisha kuwa ifikapo 2035, Morogoro itakuwa inazalisha tani elfu 20 za karafuu.
"...Sisi tukipanda miche isiyopungua milioni 2 ya mikarafuu, Morogoro, yaani, utakuwa unasema mzalishaji namba moja wa karafuu duniani ni Indonesia, namba mbili ni Morogoro – na inawezekana...," amesema Mhe. Adam Kighoma Malima.
Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amewataka wafanyabiashara pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo mkoani humo kubuni na kutumia fursa zinazotolewa na kilimo cha viungo na matunda, kwa lengo la kuutangaza amkoa wa Morogoro kimataifa kupitia uzalishaji wa mazao hayo.
Pia, ameeleza kuwa wadau wa biashara wanapaswa kubadili mtazamo kuwa kilimo si chaguo la mwisho bali ni eneo muhimu la kiuchumi linaloweza kuinua maisha ya mwananchi mmoja mmoja, na kuchangia kwa kiasi kikubwa uchumi wa taifa.
Naye Mwenyekiti wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Mkoa wa Morogoro, Muadhini Mnyanza, ameeleza kuwa chemba ya biashara mkoani humo inaendelea vizuri na kuimarisha ushirikiano na mahusiano na sekta mbalimbali ikiwa ni sehemu ya mikakati ya pamoja ya kukuza uchumi wa mkoa huo.
Kwa upande wake, aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Gairo ambaye ni Mkuu wa Mkoa mteule wa Mkoa wa Songwe, Jabiri Makame, amebainisha kuwa wilaya ya Gairo imeanza kutekeleza majaribio ya kilimo cha parachichi na viazi mviringo kwa lengo la kuendeleza ajenda ya mkoa ya kuifanya Morogoro kuwa kituo cha kilimo cha kisasa.
Nao baadhi ya wafanyabiashara wa Mkoa huo wamebainisha kuwa changamoto wanazokumbana nazo ni uhaba wa malighafi na kukosa mitaji jambo ambalo linasababisha baadhi ya viwanda kushindwa kuendelea na uzalishaji huku wakibainisha changamoto za kucheleweshwa upatikanaji wa hati miliki pindi wanaponunua maeneo ya kuwekeza.
MWISHO.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.