Maadhimisho ya miaka 80 ya Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Morogoro yaliyofanyika mwezi Mei, 2025 yameanza kuleta mafanikio kwa wadau mbalimbali kujitoa kwa hali na mali kufanya ukarabati wa majengo ya zamani ya hospitali hiyo na kuleta mabadiliko ya utoaji wa huduma kwa wananchi.
Kauli hiyo imebainishwa hii leo Juni 24, 2025 na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Best Magoma wakati wa makabidhiano ya jengo la kliniki maalumu za kibingwa lililofanyiwa ukarabati na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) ikiwa ni matokeo ya maadhimisho ya mika 80 ya hospitali hiyo ambapo wadau mbalimbali wameendelea kutoa ushirikiano kukarabati majengo yake.
Dkt. Best magoma amesema, Serikali imendelea kutoa fedha nyingi kwa ajili ya kununua vifaa kama vile X - Rays Machine, CT - SCAN, ujenzi wa jengo la mama na mtoto, jengo la dharura na kuajiri wataalamu bobezi wa afya jambo ambalo amesema limeenda kuboresha utoaji wa huduma za afya na kukidhi mahitaji ya wakazi wa Mkoa huo na maeneo jirani.
"..Ofisi ya Mkuu wa Mkoa ilikuwa mstari wa mbele kuiongoza Hospitali ya rufaa ya Mkoa katika maadhimisho ya mika 80, tunamshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kuweza kuhamasisha wadau mbalimbali.." amesema Dkt. Best magoma.
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospital hiyo Dkt. Daniel Nkungu amesema, ukarabati wa jengo la kliniki maalum za kibingwa umegharimu zaidi ya shilingi milioni 20 na lengo la ukarabati huo ni kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi kupitia ubora wa jengo hilo.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi Dkt. John Mduma amesema Serikali kupitia sheria za mashirika binafsi imeweza kuweka sheria ya kurudisha kwa wananchi "Community Socila Rensponsibility" (CSR) ambapo wao kama WCF wameweza kutoa fedha hizo za ukarabati wa jengo hilo ili kusaidia maendeleo katika sekta ya afya.
Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) ndio mdau mkubwa katika kuchangia ukarabati wa jengo hilo la kliniki maalum ya kibingwa na juhudi kubwa zilifanywa na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima katika maadhimisho ya miaka 80 ya hospitali hiyo kwa kuwashawishi wadau wa maendeleo kusaidia kutoa fedha za ukarabati majengo hayo.
MWISHO.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.