Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Kighoma Malima, ameendelea na juhudi za kutafuta njia mbadala ya kupata maji safi na salama kwa ajili ya wananchi wa mkoa huo akianza na halmashauri ya Manispaa ya Morogoro ambayo maji imekuwa ni kero kubwa na ya muda mrefu kwa wananchi wa Manispaa hiyo.
Mhe. Adam Malima hivi karibuni aliunda kamati iliyoshirikisha wajumbe kutoka taasisi mbalimbali ikiwemo Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Morogoro (MORUWASA), Bodi ya Bonde la Wami - Ruvu, Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) pamoja wa wajumbe kutoka Ofisi yake lengo likiwa ni kutafuta njia mbadala ya kumaliza kero ya maji katika halmashauri ya Morogoro ikiwemo uchimbaji wa visima.
Mnamo Juni 20, 2025, maono na juhudi hizo za Mkuu wa Mkoa zilianza kuzaa matunda baada ya kutembelea na kukagua zoezi la kuflashi maji kwenye kisima kimoja wapo chenye urefu wa mita 120, kinachoweza kuzalisha maji lita elfu 40 kwa saa na kitahudumia wananchi zaidi 100,000 kati ya wananchi 250,000 wenye shida ya maji ndani ya Halmashauri hiyo.
Akizungumza baada ya kujionea mwenyewe upatikanaji wa maji hayo, Mkuu wa Mkoa Adam Malima amewataka wananchi wa eneo la Mafisa yalipogundulika maji hayo kuyaachia maeneo yao na kutoa ushirikiano wa kutosha katika kufanikisha azma hiyo ya kupata maji kwa faida ya jamii nzima huku Serikali ikiendelea na uratibu wa kuwatafutia fidia ya nyumba na viwanja vyao.
"...Siwezi kuacha mtu analima mahindi hapa halafu Mafisa nzima haina maji, na mimi naweza kuchimba maji. Nikasema, mimi ndiye Mkuu wa Mkoa; lawama zote nitazibeba mimi. Chimbeni maji," amesisitiza Mhe. Adam Malima.
Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa amewaagiza wataalamu kujenga tanki la maji katika eneo hilo la Mafisa ili kuhudumia wakazi wa eneo la Mafisa, Kayenzi, na maeneo ya jirani, huku akitoa rai kwa wananchi kutunza chanzo hicho cha maji na miundombinu yake itakayojengwa eneo hilo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa MORUWASA, CPA Sais Kyejo, ameahidi kuendeleza ushirikiano na kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa mafanikio, pamoja na kuahidi kutekeleza maelekezo ya Mkuu wa Mkoa huku akiwahakikishia wananchi kuwa Mradi huo unalenga kuongeza vyanzo vya maji na kuboresha huduma ya maji kwa wakazi wa Manispaa ya Morogoro.
Naye Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Miundombinu Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Ezron Kilamhama, amesema uchimbaji wa kisima hicho katika eneo hilo unaonyesha uwezekano wa kuchimba visima vingine viwili, na hivyo kufanya jumla ya visima vitatu jambo ambalo litapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya upatikanaji wa maji katik manispaa hiyo.
MWISHO.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.