Kikao cha Baraza Maalum la Madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Mlimba kimeibua hoja ya upungufu wa watumishi wa Serikali wa sekta ya Elimu na Afya wilayani humo ambapo sekta ya elimu ina upungufu wa walimu 800 kwa shule za msingi na Sekondari sawa na asilimia 41 na Sekta ya Afya ina upungufu wa watumishi zaidi ya 500 sawa na asilimia 70 ya upungufu wa watumishi wote.
Hayo yamebainishwa Juni 10, 2025 na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Kighoma Malima, wakati wa kikao Maalum cha baraza la madiwani cha kupitia na kutathmini hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ili kuzipatia majawabu hoja hizo.
Akieleza zaidi Mkuu huyo wa Mkoa amesema changamoto hiyo inakwamisha utoaji bora wa huduma kwa wananchi ambapo baadhi ya shule wilayani humo zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa walimu hali inayoathiri kwa kiasi kikubwa maendeleo ya wanafunzi na utoaji wa huduma za Afya.
Hivyo ameitaka Menejimenti ya Halmashauri hiyo kuendelea kufuatilia utekelezaji wa mapendekezo ya CAG kwa ukaribu na kuweka mikakati madhubuti ya kudhibiti mapungufu hayo na kuhakikisha huduma kwa wananchi hazikwami kwa kuwa suala la rasilimali watu ni la kipaumbele.
"..menejimenti mkasimamie kwa kushirikiana na ofisi ya Katibu Tawala Mkoa kujenga hoja ya pamoja ili kupata watumishi hao.." amesema Mhe. Adam Malima.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba Mhe. Innocent Mwangasa amesema Halmashauri hiyo kwa miaka mitano mfululizo imeweza kupata hati safi hivyo amemshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendele kutoa fedha kwa ajili ya maenendeleo ya Halmashauri hiyo.
Aidha, Diwani wa Kata ya Mbingu Mhe. Nestory Kilula amesema kwenye sekta ya Afya wanaupungufu wa vifaa tiba na wataalamu wa afya jambo linalopelekea wananchi kushindwa kupatiwa huduma mahususi kwa wakati, hivyo amemuomba Mhe. Rais kuongezewa wataalamu wa Afya kwenye vituo vya Afya na zahanati ili waweze kuwahudumia wananchi pasipo na dosari.
Naye Diwani wa Kata ya Kalengakelu Mhe. Martha Daniel amesema upungufu wa walimu katika shule za Msingi na sekondari kunapelekea walimu kuzidiwa na wingi wa wanafunzi jambo linalopelekea wanafunzi kukosa umakini katika kupata elimu hivyo ameiomba Serikali kuhakikisha wanatatua changamoto hiyo.
MWISHO.
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.