Wajumbe watano wa Bodi ya chama cha Ushirika Mkoa wa Morogoro (MOFACU) kwa kushirikiana na Meneja wa Chama Kikuu cha Ushirika huo wamefikishwa kwenye Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kwa tuhuma za kuuza mali za ushirika huo bila kufuata taratibu wa Ushirika huo.
Watuhumiwa hao wamechukuliwa hatua hiyo kufuatia uchunguzi ulioanzishwa kuhusu uuzaji wa ghala la chama hicho kwa bei ya chini ukilinganisha na thamani halisi, pamoja na uuzaji wa vyuma chakavu bila kuthaminisha mali hizo.
Akizungumza Juni 7, 2025, katika kikao cha uchaguzi wa wajumbe wapya wa MOFACU kilichofanyika katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro, Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Morogoro, Bi. Cesilia Sostenes, alieleza kuwa uuzaji huo ulikiuka muongozo wa mwaka 2024 unaoelekeza mali za ushirika kuuzwa baada ya kupitishwa na mkutano mkuu, kuthaminiwa, na kupata kibali kutoka kwa Mrajisi.
"Mali hii imeuzwa na wajumbe wa Bodi bila kufuata taratibu. Tunaendelea kufuatilia kwa sababu kesi ipo TAKUKURU kwa ajili ya uchunguzi kama kulikuwa na mazingira ya rushwa ili hatua ziweze kuchukuliwa," alisema Bi. Sostenes.
Kwa mujibu wa mthaminishaji wa mali, ghala hilo lilikuwa na thamani ya shilingi milioni 126 lakini liliuzwa kwa shilingi milioni 56 tu. Aidha, vyuma chakavu viliuzwa kwa shilingi milioni 6 bila kufanyiwa uthamini.
Mwakilishi kutoka Chama cha Ushirika cha Msingi Dakawa Bwakila Amkosi, Bw. Salum Mohamed, alieleza kuwa ghala hilo lilipendekezwa kuuzwa kwa kufuata sheria zote ili fedha itakayopatikana ilipe chama cha ushirika cha zamani. Hata hivyo, kama limeuzwa bila utaratibu, ni kosa.
Naye mwanachama wa MOFACU, Bw. Mohamed Salum, aliwakumbusha wanaushirika umuhimu wa viongozi kushirikisha wanachama wote wa chama ili kupata maoni na kujua kuwa mali inauzwa na kujua bei inayotakiwa kuuzwa ili kuepusha ubadhirifu wa mali za wanaushirika.
Watahumiwa wanaendelea kuhojiwa na TAKUKURU ili kujiridhisha ukweli wa jambo hilo.
MWISHO
Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Morogoro
Sanduku la Posta: S.L.P 650 MOROGORO
Simu: +2550232934305
Simu: +255766828252
Barua pepe: ras.morogoro@tamisemi.go.tz
Haki Miliki © 2024 Ofisi Ya Mkuu wa Mkoa Morogoro. Haki Zote Zimehifadhiwa.